Tuesday, November 1, 2022

Urithi wa umaskini

Mathalani watu wachache wanaweza wasijue kama ambavyo utajiri unarithishwa basi ni hivyo hivyo kwa umaskini, ndiyo umaskini unarthishwa kutoka kizazi kwenda kizazi laba kwa kujua kwa kutokujua basi jamii hurithishana umaskini.

kama una kumbukumbu nzuri za namna matajiri huwarithisha watoto na vizazi vyao utajiri basi ni hatua zilezile pia maskini huzitumia kuwarithisha watoto na vizazi vyao. Mtizame tajiri wa migodi pale Mererani ,pengine atamchukua moja ya mwanafamilia yake na kwenda nae japo kutizama ni kwa namna gani madini yanapatika kwa kila hatua, atamhubiria juu ya namna ambavyo ataweza kunyakuka kimaisha endapo atafanya juhudi na kutumia maarifa sahihi kuyafikia madini, atasaidia kuonesha ugumu na urahisi wa kuayafika malengo na kubwa zaidi ataonesha mfano wa mafanikio japo kwa mtazamo wa maisha yake na vile anavyovimiliki.

Mfano huu utampa kiu ya mafanikio au hamu ya kumiliki mali mlengwa. Japo hatuhesabu pesa kama mafaninikio ila ni kiungo katika viungo muhimu vya mafanikia hilo halikwepeki. Pengine kwa miongo kadhaa mwanafamilia huyu atatamani naye aanze kufanya jambo japo kwa udogo ili kunyanyua hatua na atafanikiwa. Hata kama hili halitafanikiwa ataweza pata msukumo wa kufanya jingine lengo tu kufika pale ambapo tunaamini ni kiu ya kipato.

Mara kadhaa familia zenye utajiri hasa wa kipato huwa ni mfano mzuri kwa vizazi vyao, licha ya yote lakini maongezi na matendo yanayoendelea katika familia kwa kiwango kikubwa yatasadifu na kufunza utajiri.

Yote hayo yanategemea sasa tajiri huyu wa kipato ametokea wapi na je amelelewa katika namna ya kipato?Ni maswali mepesi sana ambayo yatafikirisha endapo mtu angetaka kufikiri. Ni mara chache sana kwa aina ya watu waliolelewa kimaskini (sio maskini) kuishi maisha ya kitajiri kuanzia nafsi na matendo. Changamoto nyingi zinazikumba jamii zetu hasa za kiafrika kuaminisha kwamba umaskini ni sifa au ni unyonge na udhaifu. Mathalani utamsikia mzee alielelelewa maisha duni akisema ''Ona vijana wa sasa ni wavivu sana,zama zetu tulikua tukitembea mpaka kilomita ishirini kutafuta maji ila ninyi umbali kidogo tu mtataka kupanda gari''. ukweli ni kwamba kutembea umbali kwa muda mrefu si jambo jema hasa endapo shughuli au jambo husika linapaswa kufanywa kwa haraka. Kwa ajili ya maendeleo na mapinduzi ya kisayansi na kiuchumi mambo mengi yamerahisishwa na ndio maana ya maendeleo. Hatupaswi kuishi zama hizo wala kuvifanya vizazi viishi zama hizo. Vilevile si vema kuuhubiri umaskini kama jambo la kujisifu au jambo bora ni busara kuukana na kuuepuka.

Kama mzazi au mlezi katika familia anapaswa kuhakikisaha kwa familia inapata mahitaji muhimu kwa kadiri ya uwezo wake huku akiendelea kuulani na kujaribu kila namna ya kuuepuka umaskini. Pengine wengi hawana uwezo wa kuwapatia watoto wao kila ambacho wanakihitaji ,na wengine huenda mbali hata kile kidogo alichonacho pia hatokitoa kwa familia kwa kusema kwamba ''mbona sisi tuliishi maisha magumu''. Si busara kuyaletekeza mabaya ambayo pengine yalikua ni sehemu ya historia ya mtu binafsi na kuyapeleka vizazi vya mbele,ni wajibu wa kila mmoja kuhakikisha familia yake inaishi maiisha bora na ya stara kwa kadiri yake.

Katika mzunguko wa maisha pengine ukakutana na mtu wa makamo mwenye uwezo na kipato na anagombania chakula kidogo, pengine ukakutana na mtu ambaye hapendi kuona wenzie wakipata walau kwa uchache atafanya kila hila kulikwamisha. Endapo utafuatilia hili utakuta pengine mtu huyu alilelewa kimaskini kwa kuoneshwa ugumu wa maisha na kwamba kila mmoja lazima apitie magumu hata kama ugumu hakuna.Jambo hili linapelekea kupatikana kizazi cha watu wachoyo,wenye husda na visasi kupitiliza.

Ieleweke kwamba umaskini ni jambo ambalo yeyote katika watu anaweza kunasibiana nalo na hakuna anaependa kuwa nalo,rai ni kwamba hatupaswi kuhubiri umaskini kama jambo sawa katika maisha ya mwanadau au kuishi katika hali ya umaskini hata kama hapana haja ya kufanya hayo kwani ndio maana halisi ya kurithisha umaskini.

Tukutane katika makala ijayo ili kuendelea kujengana.

Imeandaliwa na:

Abdallah Wihenge 

Mkufunzi wa masuala ya kitaasisi na tabia



Sunday, May 10, 2020

Si lazima ufanye kila biashara


Imeandikwa na Abdallah Wihenge 

Kutokana na changamoto za ajira ambazo  zinazikumba nchi nyingi hasa  za ukanda wa Afrika pengine na maeneo mengi duniani ,pamekua na mihehemko hasa kwa jamii maskini juu ya kujikwamua kutoka katika wimbi la ukosefu wa ajira na kipato.

Changamoto hii imepelekea wengi katika vijana pengine na watu wengine wakijikuta kwa kupapasa tu na bila kutumia nyingi katika fikra zao kutafakari juu ya nini na wakati gani wafanye nini. Suala hili limepelekea watu wengi kujikuta kila fursa au inayoitwa fursa basi na yeye ataingia kwa kiu tu ya kupata kipato au ujira ili kujikwamua kitoka kaika wimbi la umasikini.

Katika makala hii nitagusia maeneo kadhaa katika utimamu wa kuchagua fursa za kibiashara na kijarisiamali. Na ikumbukwe kwamba kila mtu ana kusudi katika maisha kwa maana sababu ya kuwepo kwake, na ndio maana binadamu wote hawawezi kufanya kila kitu na kila jambo. Hii ina maana hatokuwepo mtu wa kuwa mwalimu yeye, daktari, mkulima, mvuvi, mkandarasi kwa wakati mmoja..

Katika makala zilizozopita zilieleza wazi juu ya kusudi la maisha , na ni kupita makala hizo na nyinginezo utajua nini kusudio la maisha yako na kuanzia hapo utapata njia ya kusonga na kupiga hatua katika maisha kwa kujua wewe ni nani na unataka kufanya au unatakiwa kufanya nini duniani.
Katika harakati za kujikwamua kila mmoja ana namna ya kipekee ambayo anaitumia kuelezea namna ya kujikwamua.Mathalani  yapo makundi yanaamini katika biashara ya mtandao na faida zake katika kujikwamua,wapo watu wanaamini juu ya biashara ya kilimo na mazao na wanaijua jinsi ilivyo, biashara ya udalali ,vifaa vya umeme na nyingine nyingi.
Hizo zote ni biashara nzuri ila ikumbukwe kwamba si kila biashara ni ya kila mtu kuifanya,hata kama ni rahisi kiasi gani. Zingatia mambo yafuatayo unapochagua aina ya biashara ya kufanya.

  • Haijalishi ni ushawishi kiasi gani unapewa na mtu au mtu juu ya kufanya biashara husika.Fanya kile ambacho unakiamini hata kama hakuna anaekiamini.Kuna watu wana uwezo mkubwa sana wa ushawishi na kutia moyo hata kukufikisha pahala ukaona upande chanya wa jambo na kujikuta unaingia.Ushawishi hasa kwenye jambo la kibiashara ni vyema sana ila washawishi wanapaswa kujua kwamba watu wanatofautiana kati ya mtu mmoja na mwingine.
  • Ili uweze kufanikiwa katika jambo lolote ama ni zuri au baya ,hatua ya mwanzo kabisa ni kuliamini kutoka ndani ama kwa kuambiwa ama kwa kulitafakari mwenyewe.Isitoshe tu kupokea ushawishi kutoka kwa watu na ukakubali eti kwa kuwa umeambiwa ni zuri,kumbuka kuchukua muda wakao kulitafakari na kujiuliza maswali na majibu juu ya uhusiano wake na kusudio lako.
Wengi wamejikuta wakiangukia katika kila biashara na kupoteza pesa kwa changamoto ya kuparamia na ushawishi wa hali ya juu katika biashara fulani fulani.Mfano katika miaka ya hivi karibuni wakina dada wengi waliopo kwenye ajira rasmi na wale waliojiajiri wamejikita katika biashara ya mikoba na vipodozi. Ni biashara nzuri ndiyo ,Ila wengi waliojikita katika biashara hii ni kutokana na msukumo kutoka kwa marafiki pia na mitandao.Hii inapelekea katika sehemu moja ya kazi pengine yenye watu kumi basi watatu wanafanya biashara inayofanana jambo ambalo linapelekea kujidumaza kibiashara na kipato pia kwani mzunguko wa wateja ni ule ule.
  • Pia mlipuko wa biashara ya mtandao ya kwamba, njoo na mtu utapata kiasi fulani kwa uwepo wake. Hii ni moja ya biashara nzuri pia na inafanyika maeneo mengi duniani.Changamoto ni kwamba waelezeaji wa biashara hii huelezea upande mmoja tu wa biashara ,upande wa kupata na wanaacha changamoto na madhira yake nyuma.Ni vema kabla ya kuingia katika bishara hii mbali na ushawishi na msukumo mkubwa kupata muda wa kutafakari na kujiridhisha na kujifunza kwa waliowahi kufanya katika meneo mengine na walifanikiwa kwa kiasi gani.

Wengi wamepoteza pesa na wengi wapo kwenye mapambano ya kurejesha kiasi cha pesa walichowekeza bila kujua hatma yake.Wengi hujikuta wanakomaa na kuendelea kupambana na kuupoteza muda kwa kutaka kuhakikisha kiasi cha pesa kinarejea na anaendendea kupoteza fursa nyingine kutokana na mkwamo huu huu. 

Ni hivyo hivyo katika biashara nyingine kama kilimo, ufugaji, uwekezaji na kadhalika. Si vibaya kushindwa kwani ni kujifunza ila kushindwa katika jambo amabalo haukuiruhusu akili yako kutafakari ni kushindwa kiwango kibaya zaidi.
  • Usichague biashara kwa kigezo cha kujipatia pesa (nyingi) tu.Ni kweli misukumo mingi ya watu juu ya kufanya biashara ni kuhakikisha wanapata pesa za kujikwamua kiuchumi tu.Biashara au shughuli unayoifanya inapaswa kukupelekea kupata kipato cha kujikwamua ,ila jambo hili likibaki kama ndio lengo kuu na la pekee la kufanya biashara husika, basi kwa asilimia 50 tegemea kutofanikiwa na kuanguka.Wengi waliingia kwenye biashara kwa kushawishiwa na uchu wa kupata pesa. Pesa ni zawadi inayokuja baada ya kufanya jambo jema na sawa, na baada ya kufikia kusudio la maisha yako.Unaonaje kupata pesa kutoka katika kitu au biashara unayoifurahia? Utajisikaje kupata pesa katika jambo ambalo unaona asubuhi inakawia kufika ili ukafanye?Unaonaje kuutumia usiku na mchana wote kufanya kitu ambacho unakipenda na kinakuletea pesa zinazoyafanya maisha yako?
Hii ndio tafsiri ya aina ya biashara na shughuli ya kukupatia kipato unayopaswa kuifanya.

  • Jamii hasa vijana imejikuta katika wimbi la kufanya biashara kwa ajili tu ya kujionesha kwa watu kwamba nao hawajakaa bure kuna biashara ‘mishemishe ‘ wanafanya mjini.Jambo hili linapelekea kujikuta wameangukia kwenye biashara yoyote ,na hatma yake ni kuanguka na kushindwa kujikwamua kiuchumi. Hakuna anaejali ni nini unafanya hali ya kuwa hakina manufaa au hakina tija kwako au kwa jamii yako. Unahitaji kukaa chini  kutafakari na kuchanganua chochote ambacho unakitizamia kukifanya ili kikuletee kipato.Ni ngumu kufanikiwa katika jambo usilolijua ama kwa bahati nasibu ambayo nayo haitakuja mpaka uwe katika mazingira ya kuipata bahati.

  • Kuiga toka kwa watu, Hili pia ni janga kubwa hasa kwa jamii ya wazawa wa ulimwengu watatu. Mathalani elimu tuliyoipata na jamii tulizotokea hazikutuandaa kuweza kufanya maamuzi ya biashara gani au shughuli gani ya kipato yatupasa kuifanya. Hii inapelekea kuiga kwa ‘sisisi’ kutoka kwa watu wanaofanya aina fulani ya biashara. Mfano bwana fulani alifanikiwa kwa biashara ya duka la rejareja mtaani kwake , na kijana mwingine wa mtaa mwingine akaona mafanikio hayo na agharabu ana mtaji wa kumuwezesha kufanya aina hiyo ya biashara husika basi bila ya kufanya tafakari kwa yakini ,anachokitizama mbele yake ni mafanikio na sasa anakwenda kujikita katika biashara hiyo , na pengine katika mazingira yasiyo sahihi ama mbinu zisizo sahihi na anaanguka. Ni vema kujifunza na kujihakikishia juu ya kile unachotaraji kukifanya.

  • Maamuzi ya biashara moja kwa wakati mmoja ni bora zaidi kwa kuanzia.Changamoto nyingine inayowagharimu watu wengi ni kufanya mambo mengi kwa wakati mmoja.Utaona ajabu unakutana na mtu ndani ya mwezi mmoja ameshafanya takribani biashara tatu na mbili zilikwishashindwa na moja ndio anayoifanya na inaelekea kushindwa.Pengine ni tamaa au shauku ya kufanikiwa ndio msukumo wa hadha hii.Moja ya jambo kubwa ni kuweza kuwa na uwezo wa kusimamia akili binafsi.Kufanya biashara nyingi kwa wakati mmoja inapelekea kukosa kumakinika katika wazo moja la biashara na pengine maisha kwa ujumla. Kutumia muda mwingi kupigania wazo moja ni bora zaidi ya kuutumia muda huo kufanya mambo mengi yasiyo na tija.

  • Kujijengea uwezo wa kuyachanganua na kuyafanyia kazi maudhui ya wahamasishaji “motivational speakers”
Hawa ni watu muhimu sana na wamekuwa ni msaada mkubwa sana katika kutia chachu ya kuwaamsha watu katika suala zima la maendeleo na kujikwamua, pia ni wazi kwamba wao hufanya shughuli zao kwa makundi ya ujumla hali ya kuwa uwezo wa uchanganuzi na uelewa wa watu unatofautiana.Watu wengi husikiliza maudhui yanayokuja mbele zao hasa juu ya masuala ya biashara na kwa sababu wamehamasika basi hunyanyuka na hamasa na kufanya maamuzi ya kufanya chochote katika biashara, na pale hamasa inaposhuka anajikuta kumbe alichagua biashara kwa mihehemko ya hamasa na alisahau kuushirikisha ubongo wake katika maamuzi. Ni vema kuweka nukta na kutafakari kwa kina kila ambacho unahamasishwa nacho na baadae kuamua maamuzi ambayo hautajutia. kabla ya kuamua maneno mazuri ya wahamasishaji:
1.      Sikiliza na kwa makini maudhui yao
2.      Tenga muda wa kutafakari na kuamua
3.      Amua kwa moyo mmoja maamuzi yaliyo sahihi.

Changamoto nyingi katika maamuzi ya biashara ni shinikizo la hali ya maisha. Ni wazi kabisa uchumi wa dunia umekua na shinikizo kubwa kiasi cha kwamba walio na mawazo makali na mawanda mapana ya kufikiri ndio wanaweza kupambana na shinikizo hilo na kufanikiwa kimaisha hasa kupitia biashara,wenye mawazo legelege na wasiotaka sulubisha akili zao wamebaki kutizama na kubeza au kuamini kwamba kuna watu maalumu wa kufanya mambo ambayo wao wangeliweza yafanya.

Tofauti na miaka ya nyuma kufanya biashara katika zama hizi kunahitaji akili nyingi na maarifa makubwa ya kuweza kufanikiwa.Haitoshi tu kuuza na kununua kama ilivyokuwa zamani, dunia ya sasa namna ya kuuza imekua ndio kigezo kikubwa  cha kufanikiwa katika biashara na kisha bidhaa na ubora hufuata. Ndio maana utaona kuna watu wana bidhaa zisizo na ubora ila wana mauzo makubwa ,na ukweli ni kwamba wanatumia maarifa makubwa sana kuuza na kupenya katika masoko ,bila kusahau ujuzi na maarifa juu ya aina ya biashara wanayoifanya. Hautaweza kufanikiwa kwa kuparamia biashara yoyote isipokua kwa biashara unayoifahamu kwa mapana.

Pamekua na aina fulani ya watu ambao wao hufanya biashara inayo ‘trend’. Hili ni jambo zuri na ni fursa pia.Kufanya biashara ambayo inahitajika kwa wakati huo ni njia nzuri ya kukusanya kipato kwa ajili ya biashara ambayo utaishi nayo.Changamoto ya biashara za namna hii ni kukutoa katika mstari wa biashara yako ya kudumu.Hii inapoteza malengo yako ya muda mrefu na kujikuta unakwenda kutumia nguvu,akili na mali nyingi kupambana na jambo la msimu na kisha baada ya hapo unarudi kuanza moja katika biashara ya kudumu.Mara nyingi biashara hizi hufanywa na kila mtu na faida yake huwa ni ndogo ukilinganisha na rasilimali zitakazowekezwa.

Muda ni mali na ni vyema kuutumia kuboresha jambo kuu la msingi kuliko kushughulika na mambo madogo madogo yanayotumia rasilimali muda zaidi.
Katika Makala zitakazofuata tutatizamia namna gani ya kuanza kidogo katika biashara kwa kutumia mtaji kidogo na maarifa mengi,

Tuesday, August 20, 2019

Makala: kusudio la maisha ni njia ya mafanikio yako


Imeandikwa na Abdallah Wihenge | Dodoma


Siku kadhaa zilizopita nilipata fursa ya kumsikia moja ya wazungumzaji mashuhuri sana Chris Mauki katika ukanda wetu wa Afrika mashariki katika kipindi cha redio na alikua akielezea jambo juu ya kuwa na maono,mipango na kujituma  ama kujiongeza kwa kwenda hatua ya ziada katika mambo ya kimafanikio. Katika msingi wa maelezo ya mzungumzaji alielezea juu ya umuhimu wa kujitafakari na kujenga picha kubwa ya maisha yajayo na hii hainzii ukubwani ni jambo ambalo linakita mizizi tangu katika kipindi cha makuzi.
Kwa mantiki hii ni wazi kabisa wengi katika jamii nyingi za watu weusi wamekwishakawia katika kutekeleza makusudi ya maisha yao na wengi wanajikuta wanaongozwa na mfumo na kasi ya maisha na si wao ambao wanaoendesha maisha yao. Matukio na misukumo tu ya maisha ndo humfikisha mtu mahala Fulani ama pakubwa au padogo inategemea tu na ‘zali’ lake.

Ujasiriamali ni kichaka kipya cha kukimbilia?
Kulingana na hali ya maisha imekuwa utamaduni au mazoea sasa hivi watu kujificha kwenye kichaka cha ujasiriamali pale ambapo kila kitu kimekwenda mrama. Mfano kijana amesoma na akakosa ajira basi ataingia kwenye kichaka cha ujasiramali,mtu akapigwa na maisha vilivyo basi nae kichaka hiki humuhusu. Kwa maneno yasiyo rasmi tunaweza kuita ujasiriamali ni neno jingine la ukosefu wa ajira. Na mkwamo huu ni kiashiria tosha kwamba wengi ya watu katika jamii zetu  hawafahamu kusudio la maisha yao. Ni maelekezo na mfumo tuliopewa ama na wazazi,walezi au jamii juu maisha. Wengi ya wanajamii hawaishi maisha yao ndani ya kusudio isipokua mfumo ulioweka na jamii na familia.
Katika kukielezea kichaka hiki cha ujasiriamali na biashara, moja ya waandishi mashughuli wa masuala ya biashara na ushirika aliwahi kuandika “Kwa miaka ishirini iliyopita, anaelezea jinsi kila siku, zaidi ya mawazo elfu mbili hujaribu kuanzishwa kama biashara, lakini kwa mwaka mmoja, ni asilimia tano tu ya kampuni hizi zilizosajiliwa zinaishi na kukua”
Swali likazuka kichwani mwangu kwa nini sehemu kubwa sana inashindwa? Na katika maelezo yake mbeleni alieleza kuwa wengi huanzisha biashara au shughuli nyingine ya kipato kwa kusudio lisilokua rasmi yaweza kuwa ama kwa msukumo au kwa lengo la kuvuka kipindi Fulani cha maisha au msukumo toka kwa watu na kuaminishana kwamba aina fulani ya biashara na hapa sasa hufuatiwa na jaribio la biashara na si biashara.
Katika mazingira niliyoyataja hapo awali ni wazi kwamba wengi watu wengi hivi sasa hawana mpango,mkakati wala kusudio la maisha yao isipokuwa ni maisha yenyewe ndio yataamua wao wawe nini.

Kusudi la kuandika Makala hii fupi ni katika kuona ni kwa namna gani kuweka lengo la maisha kunaweza kukupa picha na njia ya maisha yenye mafanikio. Na ikumbukwe kwamba mafanikio si pesa tu, ni mkusanyiko wa mambo lukuki ambayo hayo tutaayandika katika Makala zitakazofuata.
Biashara, ujasiriamali na shughuli nyingine za kuendesha maisha ni matokeo ya shughuli za kusudio la maisha na uwepo wa mtu. Kila mmoja ni lazima ale chakula na kuishi maisha na vyote hivi havifanikiwi mpaka pawe na shuguli ya kuingiza kipato. Haiwezekani watu wote wakafanya shughuli moja ili kupata kipato.Kwa maana aina shughuli ya kipato hutofautiana kati ya mtu mmoja na mwingine. Kwa kuwa kila mtu ni sharti afanye kazi ndipo apate maisha ndio maana Makala hii imejikita kuelezea ujasiriamali na biashara katika mtazamo wa kufikia kusudio la maisha.
Katika umri Fulani wa maisha akili ya mwanadamu huanza kufikiria kwa namna gani ama ni shughuli gani mtu anaweza ifanya ili aweze kufikia malengo Fulani ya maisha au kujipatia kipato na kuendesha maisha.

Gundua kusudio lako la maisha sasa!
Kusudio la maisha huanzia hapa katika kuchagua nini cha kufanya na namna gani ya kufanya ndipo watu wengi hupanda kipando kisicho sahihi katika kufikia malengo ya maisha yao na kwa namna wanaweza kufanikiwa.
Kipando au njia sahihi ndiyo itakayomfikisha mtu pahala sahihi kimaisha, ila kushindwa kujua upo duniani kwa lengo gani au wewe ni nani basi kwako maana ya maisha itabaki kuwa ni pumzi. Baadhi ya watu ni matajiri wakubwa na wamiliki wa makampuni makubwa ndani yao na ndio kusudio la kuumbwa kwao ,ila kwa kushindwa tu kutambua hilo wao wamebaki kuwa masikini na mafukara wakubwa. Lewis Carol, mwandishi mashuguli wa miaka ya 1800 aliwahi kusema Ikiwa haujui unaenda wapi, barabara yoyote itakufikia “. Kwa mtazamo huu mtu asitegemee kupiga hatua ikiwa hajui kusudio la maisha yake ni nini.

Katika mchakato mzima wa kufikia kusudio sahihi linakuwepo ndani ya mtu na uwezekano wa kutimilika kun maswali yanamjuzu mtu kujiuliza na kasha kuanzia hapo ule mchakato mzima wa kuyafikia malengo ya maisha na mafanikio huanzia hapo.

·        Kitu kipi unakihitaji sana?
·        Jambo gani linakufikirisha sana?
·        Kwa namna gani unatumia pesa zako?
·        Namna gani unatumia muda wako?
·        Ni akina nani unafurahi kushirikiana nao?
·        Kipi kinakufanya ucheke?
Mambo haya yapatayo saba ni kichocheo kizuri sana katika kuyafika makusudi ya maisha na  mafanikio. Ni moja ya funguo kubwa katika kufungua makufuli na vifungo na ubongo wa kila mwenye nia thabiti ya kutaka kupiga hatua.Hakuna atakayekua na na mafanikio ya kweli isipokua yule anaefanya kitu ambacho yeye ni shauku (passion) yake kuyafanya.
Ngoja nikwambie, ifahamike kwamba mambo mengi tunayoyafanya si lengo la kuwepo kwetu isipokua kutokutambua tu ndio kunatupeleka katika lengo lisilo sahihi  la maisha na ndio tunalalama na kukosa mwelekeo yaani mbona maisha yamekwama. Baadhi yetu tunaamini tumefanikiwa mbele ya macho ya watu kwa kumiliki vitu vya thamani ila ukweli ni kwamba mafanikio ni zaidi ya hayo.
Kwa maneno yasiyokuwa rasmi mafanikio ni kuwa vile unavyopenda kuwa na kunufaika na kunufaisha wengine kwa vile unavyovipenda. Ukweli ni kwamba wengi tunatumia nguvu nyingi kutafuta vitu ili kuridhia macho ya watu au tu kusongesha maisha mbele, ila pengine hata hatufurahii kile tunachokifanya isipokuwa ni mfumo na msukumo tu wa maisha ndio unatulazimisha kuwepo hapo na hatuna namna.
Hakuna jambo bora sana katika maisha kama kufanya jambo ambalo unalifurahia na linakuletea kipato. Jambo amabalo unaingoja asubuhi ili uamke na kulifanya,jambo ambalo hautamani jua lizame kabla haujamaliza. Na hili ndilo kusudio la maisha linautosheleza moyo ,linatosheleza wengine na linaleta kipato. Kipato hufuata tena kikubwa na kwa kasi kubwa hasa unapofanya jambo sahihi kwa wkati sahihi ambalo ni kusudio la kuwepo kwako.

Upo duniani kwa lengo maalum, ligundue leo!

Kila mmoja katika hii dunia ana lengo na kazi maalumu ya kufanya ambayo hakuna mtu mwingine yoyote aliletwa kuifanya. Kama ambavyo alama za vidole (finger prints) zilivyo tofauti; basi na lengo la kuwepo kwako duniani ni tofauti na la mwingine, japokua kwa mbali sana linaweza onekana linafanana na mwingine.
Kujua lengo au kusudio la maisha yako inakupasa; kujua ni kitu gani unakifanya vizuri zaidi, watu wanapenda nini toka kwako, kitu gani una shauku nacho kila inapoitwa leo. Geuka nyuma na tafakari na kukumbuka.



1.     Ni kitu gani huwa unashauku ya kukifanya na huwa ni kirahisi sana kukifanya hata kama wengine wanakiona kigumu na wanashindwa pengine?
2.     Jambo gani unachukia sana unapoona mtu mwingine anakifanya kwa makosa wakati wewe unaweza kukifanya vizuri sana?
3.     Kitu ambacho unapenda kukifanya hata kama hautalipwa unaendelea kukipenda?

Kuna zawadi kubwa sana ndani yako itafute, ifanye iwepo ikufanyie kazi na uifurahie,itabadili maisha yako na ya wengine na hii ndio njia ya kutafuta na kupata kusudio la maisha yako.
Katika kufikia kusudio la maisha yako fuata hatua zifuatazo itakusaidia.
Hatua ya kwanza: Jenga picha ya kule unapotaka kufika.


Jione wewe uliefanikiwa yaone mafanikio yako. Hii itakusaidia kuongeza jitihada kufikia mafanikio.Picha kubwa hii unaiona katika jambo ambalo unalipenda na kuliweza. Mfano unajiona upo uwanja mkubwa unacheza mpira na timu kubwa Afrika au duniani. Endapo tu unapenda na unajua kucheza mpira. Hii itatoa hamasa ya kufanya mazoezi na kuweka juhudi katika kufikia lengo na kusudio la maisha yako ya mafanikio. Cameron Johnson mzungumzaji na mshauri wa makampuni Zaidi ya 500 makubwa duniani moja ya nukuu zake aliwahi kusema “Usiogope kukataliwa ,usitafute sababu ya kushindwa ,anza kidogo, tia mkazo kufanya mambo mazuri na kila kitu kitafuata .Kila kitu kina kujifunza na mwishowe mafanikio huja kama mfumo wa maisha”.Kikubwa ni kuanza na kufanya katika usahihi utashangaa jinsi mafuriko ya mafanikio yanavyokupata.

Hatua ya pili: Weka nguvu na mkazo katika yale unayotaka kufanya.
Chukua hatua walau ndogo ,thubutu kufanya walau kidogo,weka mikakati na usiogope kujikwaa ama kuanguka. Ni sehemu ya mafanikio kwa maana utakua umejifunza.Kwa kuwa sasa unajua nini unaweza na nini unataka na wewe ni nani.
Kwa kuwa na uhakika na hilo ,sasa unaweza kuchukua hatua maana mafanikio yako yapo ndani yako.Kumbuka ni hatua ya kwanza ndio jambo kubwa Zaidi.Haitatokea miujiza ya kufanikiwa kufikia kusudio la maisha kabla haujachukua hatua yoyote ,kwa kushindwa kufanya hivyo utabaki hapo ulipo na labda utapiga hatua nyuma.

Hatua ya tatu: Songa mbele.
Haijalishi ni ngumu kiasi gani, hakuna jambo zuri lilikuja kwa urahisi. Usiruhusu mawazo ya watu wengine yakubomoe hali ya kua unaamini kile unachokifanya ni sahihi. Kumbuka kila mtu ana historia ya maisha yake. Fikiria nje ya sanduku na amini wewe ni Zaidi ya ulivyo.Tumia akili yako yote na uwezo wako wote kulisimamisha hilo unaloliamini maana hilo ndio wewe.Katika jamii kila mmoja huwa na maoni yake juu ya kila tukio ambalo linatokea. Wapo ambao kwa mawazo yao huamini haitakaa iwezekane jambo Fulani kutokea. Ila kwa kuwa wewe unaweza na unaamini unaweza basi ni kweli unaweza.
Katika jambo ambalo upo mahala sahihi na unatia jitihada basi hata Mungu husimama nyumba yako na kukuandalia majeshi ya kukuvusha salama . Hotuba ya Mwalimu Julius Nyerere aliyoitoa tarehe 2 Novemba, 1978 alipokuwa akitangaza vita vya kupambana na uvamizi wa majeshi ya Idd Amini katika ukumbi wa Diamond Jubilee, alisema kauli ya “…………Uwezo wakumpiga tunao. Sababu ya kumpiga tunayo. Na nia ya kupiga tunayo……..”  kwa kuamini hivi ndivyo ilivyokuwa na ushindi mkubwa ulipatikana. Unapokuwa na nia sababu , na uwezo kwa nini ushindwe?

Hatua ya nne: Weka vipaumbele katika mambo ya msingi.
kila jambo unatakiwa ufanye ,si kila biashara nzuri iliyomletea mtu Fulani mafanikio basi na wewe utapata nalo mafanikio. Tengeneza mtandao wako wa watu na ushirika na watu ambao watakua na wewe katika mchakato. Moja ya mambo niliyowahi kujifunza ni kwamba unapotaka kufika mahala Fulani ikiwa ndio sababu ya uwepo wako basi kuna watu waliumbwa na wao lengo la kuwepo kwao ni kuhakikisha lengo lako linatimia, na kama haujachukua hatua basi kuna idadi kubwa ya watu wanaangukwa kwa wewe tu kutokufanya hivyo.
Wao wanatakiwa kufikia kusudia la maisha yao ila wewe ni sehemu ya kusudio lao kama wao walivyo sehemu ya kusudio lako. Unaweza kuwa na wazo pan asana na pengine wewe pekee usitoshe na unahitaji watu wa taaluma mbali mbali basi hao ndio wa kuwatumia na muweze kusafiri pamoja  kila mtu kufika kusudio la maisha yake. Mwandishi Winston Churchill aliwahi kusema ….tunajenga majengo yetu ,na majengo yetu hutujenga.” Kusudi ya kauli hii ya bwana Churchill ni kwamba kile ambacho tuanakifanya leo ndio picha halisi ya kesho yako.Fanya kazi leo ,tena kwa nguvu sana na kesho utafurahia kwa dhifa kubwa.

Hatua ya Tano: Tengeneza brand ya kusudio lako.
Kumbuka unachofanya ni cha kwako basi kifanye kwa namna yako na si kwa namna ya mwingine kuwa wa kipekee hata kama mwingine anafanya si lazima ufanye kama yeye kwa sababu yeye sio wewe. Be “you”nique.
Jifunze tena na tena ili kujiimarisha kwa unalotaka kulifanya. Kuna tofauti kubwa sana kati ya ukweli wa wewe ulivyo na nini kipo ndani ya watu wanaokutazama.Tengeneza picha yako.

Hatua ya Sita: Endelea kujiboresha leo ,kesho na kila siku.
Usijifunge hapo jaribu kukua na kufanya jambo jipya kila unapotaka au inapohitajika kufanya hivyo. Na mara nyingi unapofanya jambo ililoumbwa kwalo basi utaendlea kufanya licha ya ugumu wowote kaa tulivyosema awali kitu amabacho hata usipolipwa una nraha kufanya. Na hili litatoka kuwa jambo unalolipenda tu mpaka jambo lenye kuleta faida kubwa.Tumia teknolojia ni msaada mkubwa Kuwa mbunifu Kwa hatua hizi kwa kuwa na ustahimilivu na jitihada itapelekea mafanikio kutokea kwa wakati. Ama ni biashara au aina yoyote ya shughuli ya kupata kipato basi ona kwamba hilo ni jambo lako na ndilo unalopaswa kulifanya ndilo unalolimiliki.
Usiwe mzito katika kufanya maamuzi, kutumia taarifa zinazopatikana hata kama ni ndogo, matumizi ya muda jua ni wakati gani wa kusema NDIYO au HAPANA au KUKAA KIMYA. Jua ni wakati gani wa kujifunza, kuondoa mawazo hasi kichwani ,wakati wa kutafakari na kutafakari tena na tena.Kujiboresha ndio msingi wa kufika kusudio la maisha yako.
Kwa maneno ya Siddhārtha Gautama,mwanafalsafa ,mwalimu na kiongozi ya dini ya kibuddha "Kusudio lako maishani ni kupata kusudi lako na kutoa moyo wako wote na roho yako yote kwenye kusudio hilo"
Siddhārtha Gautama



……………………….
Mwandishi ni mkurugenzi wa Umoja Creatives Company na Mkufunzi wa Uongozi na Menejimenti. Mawasiliano: +255 716 050 555, +255 754 686 393, abbshey09@gmail.com
                                                            …………………………..